Jumanne, 16 Julai 2013

UNAYEMUACHA ANASTAHILI?



Uamuzi unaochukua leo ndiyo wenye kuweza kukusababishia furaha au majuto baadaye. Mambo mengi yaliotokea leo ni matokeo ya kile ulichokiamua jana. Iko hivyo na  Hata katika mapenzi hali ni hiyo hiyo.
    Uzuri wa mahusiano yako ya leo umeamuliwa na uamuzi mzuri wa kusikiliza hisia zako na kuamua kuwa na huyo uliye naye leo.
Huyo anayekufanya kila dakika uone thamani na amani ya kuwa katika nyumba yako. Aliyefanya mahusiano yako yawe tofauti na wale ambao Bar ni sehemu salama zaidi kwao kuliko katika nyumba zao. Ila hata wao hali waliyo nayo leo ni matokeo ya kile walichoamua jana.
    Uamuzi wako wa leo ni mbegu ya kitakachoota kesho. Ukiamua leo kuwa na mtu usiyemuamini  ni mbegu ambayo itazaa mahusiano ya wasi wasi. Uliyenaye humtaki, na unaona suluhisho pekee ni kumuacha?  
    Sijui mnavyoishi hivyo siwezi kuliongelea sana ila je, unaamini anastahili kuachwa? Sababu unazotaka ziwe kama sababu kuu za kuachana kwenu zinaingia akilini?  Mbali na hilo amekosa sifa thabiti ya kuwa na wewe? Sifa ya kukupenda kwa dhati?
   Kuachana kwenu leo kunatoa fursa ya yeye kuwa huru mbali na wewe. Uhuru utakaompa nafasi ya kuangalia mwingine bila ya nafsi yake kusutwa wala kuona hatia. Una uhakika unastahili kumuacha?
    Una uhakika kumuacha kwako si kupanda mbegu ya majuto itakayokutesa kesho? Mapungufu ni suala la kila binaadamu, kama hiyo ndiyo sababu ya kutaka kumuachia futa. Kama makosa anayofanya mpenzi wako japo yanaumiza ila anaonekana kuwa na nia madhubuti ya kuyaacha pia hastahili kuachwa. Kuacha linaweza kuonekana kama tendo rahisi, ila haliko hivyo.
   Unamuacha leo huyo uliyemzoea ambaye unajua  mapungufu yake ila mbali na yote una mapenzi naye. Unayeenda kukutana naye unamjua? Haitoshi kusema unamjua eti kisa umekutana naye mara mbili mara tatu. Si rahisi kumjua mtu vizuri kwa namna hiyo. Tabia ya mtu utajua vizuri kwa kuongea naye mara kwa mara au kwa kuishi  naye. Hapo hawezi kuigiza tena.
    Unapotaka kuachana na mtu ni vyema kwanza  utulie kwa muda  ukitafakari sababu za wewe kuachana naye na hali ilivyo. Si vyema kuachana naye wakati una hasira. Ukifanya hivyo ni wazi hautotoa uamuzi sahihi, uamuzi utakaoutoa hapo si ajabu baadaye kuujutia sana.
     Hata siku moja hasira haifai kuwa kiongozi katika kufikia maamuzi. Wengi bila kujua hili walijikuta walipogombana na wapenzi wao bila kutafakari wakajikuta wakitaka kuachana, na matokeo yake sasa wakiwaona wapenzi wao wapo na watu wengine mioyo inawauma. Kila wanapowaona wapenzi wao wanahisi hawajawatendea haki kuwa na watu wengine, bila kujua kuwa uamuzi wake ndiyo sababu ya yote.
    Ni kweli, wakati mwingine mtu unajikuta unafanya vitu bila kutarajia,ila unapoona umekosewa na mpenzi wako hebu kaa naye mbali kwa muda, ili ujipe muda wa kutafakari. Katika muda huo unaojipa ndiyo utaweza kupima ukubwa wa kosa la mpenzi wako na adhabu stahili unayopaswa kumpatia.
   Uamuzi wa kuachana haupaswi kuwa kimbilio ukifanyiwa makosa. Ni rahisi sana kuona unafanya uamuzi sahihi leo kwa kufanya hivyo ila jua unapoteza vitu vingi ambavyo havipatikani kwa urahisi.
   Unampoteza mtu unayempenda kwanza, pia unampoteza mtu ambaye angalau unamjua kwa undani. Katika dunia ya leo iliyojaa kila aina ya chanagamoto sababu nyepesi hazifai kuwa sababu za wewe kuachana na mpenzi wako.
     Kuwa mwalimu kwa mwenzako kwa yale mambo ambayo unaona anakukosea badala ya kutaka kuachana naye. Kuachana na mtu mnayependana nae leo ni kupanda mbegu ya mauvivu baadaye.
    Angalia vizuri sababu  zako za kuachana kama ni ngumu huenda kusiwe na la kufanya ila, kama ni hizi  hizi za kuchelewa kurudi bila kujua sababu we unaona hafai. Kama ni hizi za simu yake kupigwa mara nyingi bila kujua mpigaji we unakasirika na kumuona Malaya! Fikiri sana. Kupoteza ni rahisi sana kuliko kutafuta. Ahsanteni.
           ramadhanimasenga@yahoo.com



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni