Jumapili, 14 Julai 2013

HATAKI KUBADILIKA KWA SABABU HII



Uhusiano wa mapenzi ni muunganiko wa hiyari wa watu wawili wenye kupendana,kukubaliana na walio tayari kuvumiliana na kurekebishana pale inapobidi. Hiyo ni moja kati ya tafsiri rahisi ya uhusiano wa mapenzi.
    Mtu yoyote aliyekuwapo katika mahusiano anatakiwa kuwa tayari kumsikiliza mwenzake, kumvumilia na kubadilika kitabia pale inapopaswa kuwa hivyo.

   Na kwa kuwa suala la mapenzi ni suala ambalo huwakutanisha watu ambao hupendana basi mambo mengi hukuta yakienda ‘Automatically’ au bila kutumia nguvu kubwa katika kuyabadilisha. Hata kama mmoja alikuwa mlevi sana au tabia nyingine yenye kukera,basi huweza kubadilika kwa lengo la kumfanya mwenzake awe na furaha.
    Kama kweli ana upendo na wewe, kubadilika ni suala ambalo atalipa kipaumbele hata kama litachukua muda mrefu kiasi gani. Watu wenye kupendana kwa dhati hupenda kusikilizana na kuridhiana katika yale mambo ambayo huona inafaa kufanya hivyo.
    Si jambo la kawaida hata kidogo kukuta malumbano ya kila siku katika nyumba ya watu wanaopendana kwa dhati. Upendo huwafanya waishi kwa amani na masikilizano.
    Nguvu ya upendo huwafanya  hata wenye historia tofauti katika maisha kusionekane tofauti baina yao. Huwafanya wasomi na wasiokuwa wasomi wajione ni sawa. Lakini hali huwa tofauti katika nyumba isiyokuwa na upendo.
    Amani huwa shida. Ugomvi huwa karibu kila siku. Hata vile vitu vidogo ambavyo huweza kumalizwa kwa busara hushindikana mpaka kelele na maneno kadhaa ya kashfa yachukue nafasi. Kila mmoja hujiona yuko juu ya mwenzie.
  Msomi atataka kuonesha usomi wake hata pale asipoweza kufanya hivyo. Mrembo atataka kudhihirisha hilo mbele ya mpenzi wake, ilimradi tu.Kisa?
  Upendo baina yao hakuna.  Laiti kama ungekuwapo pasingekuwapo madaraja baina yao. Hakuna ambaye angejiona yuko juu ya mwenzake. Wote wangejiona sawa.
    Katika majumba mengi kuna kesi nyingi baina ya wanandoa. Kila siku kama si kuitwa mshenga basi ni safari kwenda kuomba nasaha kwa wazazi. Ndoa nyingi zinaishi kwa ajili ya busara ya wazazi na si upendo uliopo baina ya wahusika.
   Wanawake wengi wanatoa uroda kwa waume zao kutimiza wajibu tu. Wanaume wengi katika majumba yao wanawahi kurudi nyumbani kwa sababu ya kuogopa kuitwa katika vikao na wazazi. Ukichunguza chanzo cha yote utapata jibu hili.
    Upendo baina yao hakuna au umeanza kufifia. Ukiishi na mtu unayempenda si mara kwa mara kesi zenu zitahitaji hakimu kutoka nje. Mara nyingi mambo yenu mtaweza kuyamaliza ndani hata majirani wasijue.
   Kuishi na mtu ambaye aidha ulichaguliwa au ulilazimika kumuoa kufuata kitu tofauti na hisia za upendo juu yake ni janga.
   Ni lazima utakutana na tabia za ajabu na asitake kuzibadilisha. Kama alikuwa mlevi basi atakwambia alianza kulewa kabla hamjawa pamoja, hivyo usimuingilie katika maisha yake. Kama ulimkuta ni mtu wa disco si ajabu sana akikwambia muziki uko katika damu yake, kwa hiyo kama unataka kuendelea kuishi naye basi itabidi ukubaliane na kila unachomuona nacho.
   Kumjua mtu akupendaye kwa dhati wala ahihitaji shahada ya chuo kikuu. Yatazame matendo yake, angalie jinsi anavyoonesha kukujali, mwangalie jinsi atakavyokuwa anajali furaha yako. Kisha changanua kama matendo yake kwako yanakupa furaha na yanahakikisha unapata amani katika nafsi yako.
   Kutokana na wengi kulala usingizi wa mapenzi, kuna kitu huwa tunashindwa kufahamu na kujikuta kila siku tunaumia kichwa.
   Watu wengi tunaumia kichwa kuwaambia wapenzi wetu vitu tupendavyo ilhali wakiwa wanajua. Ila pia mbali na kutumia muda mwingi katika kuwaambia vitu hivyo lakini mara nyingi huwa hawavifanyi na matokeo yake kutuacha na majonzi na masikitiko makubwa. Narudia tena.
   mtu akupendaye atapenda akuone na furaha na amani. Hata siku moja hatopenda kukuona ukiumizwa na matendo yake. Acha kuumiza sana kichwa na badala yake ishi na ukweli huu.
   Kama kweli anakupenda kwa dhati angebadilika. Acha kuchosha misuli ya kichwa kila siku kwa kusema neno moja.
     ramadhanimasenga@yahoo.com



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni